Friday, January 31, 2014

Ugoya wa simba

Hebu tupumzike na maswali tupate simulizi nzuuri sana ya mapenzi




Kulikuwa na mwana dada mmoja aliolewa kwa ndoa ya kifahari sana, pia alikuwa tajiri kama malkia wa nyuki.  Basi pamoja na utajiri wake wote lakini hakuwa na furaha kwenye ndoa yake, yaani mume siku zingine anarudi usiku wa manane mara nyingine alale huko huko. 
Mwana dada akaona makubwa haya akaenda kwa mganga kutafuta dawa ya kumtuliza mumewe, alipofika kwa mganga na kumuelezea shida yake mganga akamwambia tatizo lake ni kubwa mno linahitaji apate ngoya za simba zile za shingoni. akasema hakuna shida ili mradi tuu mumewe atulie nyumbani.

Siku iliyofuata akachinja mbuzi akabeba miguu na mikono akaenda porini kumtafuta simba, akafika sehemu kuna bwawa la maji pembeni kuna mti mkubwa.  Basi akapanda juu ya mti akachukua kamba akafunga ile miguu na mikono ya mbuzi kila moja na kamba yake alafu akaining'iniza chini simba alipopita kwenda kunywa maji akadaka ile miguu na mikono akala kisha akaenda kunywa maji. 
baada ya hapo yule mwanamke akashuka akaenda nyumbani, kesho yake akafanya vile vile huku nae akishuka kwenye tawi la chini, baada ya wiki moja simba akazoea kupitia pale na Mwana dada nae woga ukapungua akashuka mpaka tawi la chini kabisa siku hiyo ile anampa tu akamvuta manyoya ya shingoni simba akatoka mbio na mwana dada nae moja kwa moja mpaka kwa mganga.

Alipofika mganga alishtuka akamuuliza amenunua wapi mwana dada akamwambia ameyachomoa mwenyewe shingoni kwa simba.  Mganga hakuamini akamwambia itabidi kesho akamwonyeshe alivyoyachukua.  Basi siku ya pili mwana dada akampitia mganga wakaenda mpaka kule porini, mwanadada akamwambia mganga ajifiche pembeni ya bwawa kulikuwa na kichaka fulani hivi.

Muda wa simba ukafika akapita pale kula nyama, mwana dada naye kama kawaida yake ile anakula tu akamkupua manyoya ya shingoni  simba akatoka mbio, na mganga kule naye mweleka haja zote zikamtoka, mwana dada kumpitia akamkuta kajichafua vibaya sana.

Nini kiliendelea tukutane kesho 



Toa maoni yako

Thursday, January 30, 2014

USALITI NI MSUMARI WA MOTO


Nimepata maswali ya wasomaji weengi zaidi ya 20 wanalalamika kuhusu usaliti wa wapenzi wao naomba niwajibu kwa pamoja ili nipunguze foleni ya maswali yenu:


Kwanza kama ulisoma mada yangu ya TALK ABOUT LOVE yote utapata majibu mazuri zaidi lakini naomba nijibu tena.

Suala la mume/mke/mpenzi wako kukusaliti inatokana na mambo mengi sana haya ni baadhi tu:

Anakupenda kweli?
Maana huenda alikupenda ajili ya kitu fulani mfano mwanaume alikupenda ulikuwa na sura nzuri, umbo namba 8 sasa umejiachia kunenepa mpaka hata alivyokupendea vimetoweka, au ajali masikini umepoteza kiungo au sura imeharibika.
Kwa mwanamke huenda ulikuwa na mali, Umaarufu au umbo zuri baadaye vikatoweka.
Anayekupenda kweli hakusaliti hata ufikwe na majanga gani.


  • Kauli mbovu
Kwa mpenzio huuwa mapenzi yote yaani anakuambia vizuri utamjibu majibu ya karaha kama adui yako, tena kwa wote maana kuna wanaume pia wana midomo michafu akikupa moja unakumbuka kwenu.
  • Chakula cha usiku 
Tena hii ni sababu kubwa kuliko zote mwanaume asipopata hiyo kitu usaliti unauita peupee na ujue akisaliti mara moja ananogewa kujirudi sio rahisi.
 Kwa mwanamke ukiona mumeo anakunyima muulize vizuri kama hujamkosea jua kuna mwenzio anamchosha maana huwa hawawezi kuvumilia bila hiyo kitu.
  • Makaribisho mabovu 
Yaani ukimuona mumeo unakuwa kama umeona gari ya taka, unakunja na sura karibu inatokea kisogoni, akipata makaribisho mazuri hakumbuki hata shati.
  • Usafi/umaridadi
Mumeo anarudi kazini anakukuta mchafu  make up au nguo nzuri unavaa ukiwa na mwaliko, 
Au we dada unaefanya kazi ukianza kwenda kazini unajipara kweli kweli, ukirudi unatafuta kanguo hakana hata sura ndio unavaa we unadhani mumeo anaona waliojipara wangapi huko nje. Na hizo nguo na vipodozi alivyonunua aishie kuona unajipara wakati unatoka inaingia akilini kweli.

Pia usafi wa kwa bibi jamani tuseme ukweli kuna wadada wengine wananuka sana, kwa sababu hawapendi kutumia maji kujisafisha, mwanamke maji ndio kila kitu, pia usisahau mwanamke ana miswaki miwili, kujipara usoni hakuna maana kama hujisafishi vizuri, hamu yote humuisha mwanaume akikuta kwa bibi kuna uvundo shost, atakupa mgongo kama hakujui.
  • Matumizi 
Yanazidi kipato kila uonacho mwanamke roho inakusimama, mumeo akisema hana pesa unauvuta mdomo, akimpata anae mhurumia umelia.

Na nyie wanaume mabahili,  mkeo hajui mapato yako, humpi chakula kizuri, mavazi anayaona yanang'aa kwenye maduka, kila siku unamwimbia wimbo wa subira, dagaa lake mchicha ndio kabisa kila siku, pesa ya matumizi unampa kila siku haitoshi hata mlo wa siku, mwanamke hana hata akiba kidogo haaa weee akimpata anayempa elf kumi tu atakusaliti lazima.
  • Ugomvi wa kila mara  
Yaani hamkai pamoja lazima majirani wazime radio kuwasikiliza mnavyogombana, hata mnachogombania hakina kichwa wala miguu, mmoja wenu akiwa hayupo cm kutwa uko wapi, unarudi saa ngapi maswali meengi kama mnapendana vile.
Ndio unakuta mwanaume akitoka kazini anakaa kwanza mahali mpaka saa nne za usiku ndio unarudi na kusingizia foleni, lakini ukweli  haoni faida ya kurudi home mapema atamaliza siku vibaya. akimpata wa kumpa raha na sio karaha zako atasahau hadi jina lako.

Jamani usaliti unaumiza sana kama msumari wa moto kwenye kidonda
 Tafadhali usimsaliti mwenzio 






Toa maoni yako

Tuesday, January 28, 2014

I love you za Facebook



Amina wa Kibaha 
Dada naomba kuuliza hivi nani alileta hii mitandao ya kijamii?
Jamani ndoa yangu inang'inia mume wangu kutwa anachat na wanawake, simu ndio usiseme hatuna muda hata wa kujadili hata mambo ya familia yetu.
Tena toka ameanza mambo ya mitandao amekuwa anaomba mapenzi haramu mi siwezi basi ananuna, nikawa najiuliza mbona zamani hakuwa na mambo haya, juzi nilichungulia kwenye laptop yake mmh nilichokiona dada mavideo ya ngono  kajaza humo, 
Natamani niondoke lakini watoto wangu bado wadogo sijui hata nifanyeje ndoa yangu naipenda ina miaka sita tuu.

JIBU
Pole sana mdogo wangu,
Mbona wengi tunatumia mitandao na ndoa zetu zipo salama salimini.

Huo ni ulimbukeni wa teknolojia mwanaume weye na wala aliyeleta hakukwambia ubebe taka zote upeleke nyumbani kwako hayo maporn unayo angalia wenzio wapo kazini wanalipwa, wanakunywa madawa,  wana madaktari wao wanapimwa afya na kila kitu we ukamfanyie mkeo  hata aibu huna.

Kwanza wana mapenzi gani kuzidi yetu ya kibantu khaa uchafu mtupu,  kinachokufanya uvunje ndoa yako nini, hao unaowaona wazuri  kwenye mtandao ni make up tuu hebu kawatembelee asubuhi uwakute ndio wanaamka kama hujatapika. Hata mkeo ukimnunulia anaweza kuwashinda hao wanao kuzuzua. Hivi hujiulizi kutwa nzima wanachat na wangapi, wangapi wanaambiwa love you kama wewe, acha umburulaaa.

Mdogo wangu usiondoke pigania ndoa yako usidhani hao wanaomzuzua ni wakaaji, wao ni wabomoaji tuu utatesa watoto wako bure shost hayo magume gume yaloshindikana na mitume yasikutishe, tena jiamini wewe ndio mwenyewe wengine wote wezi.

Pia usikubali kabisa huko anako kuomba tena uwe macho maana wanajifanyaga wamepotea njia, mwache anune kama ana uwezo akumeze kabisa ukae tumboni mwake.  Atakuharibu utembee na nzi kama unauza utumbo, kisha akubwage mchana kweupee.  Jali wanao mwaya watapata shida malezi yao yanategemea umoja wenu, akizidi mpeleke kwa viongozi wa dini. 






Toa maoni yako

Monday, January 27, 2014

Nyumba ndogo


                                          

Habari za weekend wapendwa, natumaini ilikuwa poa.
Leo nitaendelea na maswali yenu yako mengi sana nadhani mengine tutayajibu baada ya mada ijayo.

Saimon wa Kenya
Habari yako  dada mi  nina miaka 30 nimeoa, ni bibi na  tuna mtoto mmoja, simuelewi mke wangu huwa anamaanisha nini kulaza mtoto katikati yetu pia hata kama mmekaa pamoja ye hana mapenzi tena na mimi bali na mtoto sasa dada nikitafuta mpango wa kando nitakosea?

JIBU
Utakosea sana kaka Saimon, mwanaume anayejiamini hutafuta suluhu ndani ya nyumba yake, huyo nyumba ndogo atakusaidia mapenzi yarudi ndani au atazidi kubomoa.  
Na ukiamua hivyo ina maana utawatenga mama na mtoto, na nyumba ndogo zilivyo mbona utasahau kama umeoa.  Kisha huyo nyumba ndogo unajuaje kama atakuwa mwaminifu kwako? 

Ndio mwanzo wa kubeba magonjwa na kuleta nyumbani, tafadhali tulia na mkeo hayo ni mambo ya mpito, kwani mwanamke akiwa mja mzito huwa katika hali ya kuathirika kisaikolojia na ndio maana huweza muona akinuna bila sababu, wengine hulia, kuchagua vyakula au nguo, kuchukia watu wa jinsia fulani bila sababu.

Sasa hali hiyo wengine huendelea mpaka anapokuwa na mtoto hupenda kuongea au kucheza na mtoto muda wote namaanisha mapenzi yote ya baba yanahamia kwa mtoto, anasahau kuwa sasa ana watoto wawili mtoto mkubwa (Mume) na mtoto mdogo.
Pia msaidie unapopata nafasi kucheza na mtoto kila umuonapo anacheza naye, akiona hivyo atafurahi kuona unamsapoti kwa anachokipenda naye  atarudisha mapenzi kwako.
   
Ok bye



Toa maoni yako

Saturday, January 25, 2014

Mapenzi ndoa - i love you kelele tuu







Halima wa Dar

Shikamoo Dada mi ninauliza hivi
Nina bwana ninaishi naye mwaka wa 5 sasa kila nikimwambia kuhusu ndoa anakuwa mkali na kuniuliza kwani nimepungukiwa nini, 
nami ninaamini tukifunga ndoa itanipa kujiamini pia kuishi hivi tunamkosea Mungu nifanyeje dada?

JIBU
Mmh jamani naomba usikwazike kwa majibu yangu,
Kosa la kwanza ni  kitendo cha wewe kwenda kuishi na mwanaume bila mwanaume kukamilisha taratibu,
umejirahisi kupita kiasi my dear, tena hata familia yako sina uhakika kama ilifurahia, kwani furaha ya wazazi ni kuona binti yao anafuata maadili .   Hee inakuwaje kwani utoke kwenu kwenda kuishi na mwanaume hivi hivi duuh kiasi yakukute. 







Kwa mila za kiafrika sijui mabara mengine ni mwanaume ndio anaesumbuka ili kukupata.  Sasa we ulipojippeleka ukamrahisishia kazi ndio maana haoni umuhimu wa ndoa, japo ni muhimu sana katika kujenga familia bora na kuanzisha ukoo.

Pili mwanzo wakati unaenda kuishi naye hukujua kuwa ni dhambi sasa baada ya kuona ndoa inaota mbawa umemkumbuka na Mungu, ni vizuri kumkumbuka Mungu kabla hujafanya jambo lako lolote.

Kisha hawa wanaume wengi wanatuliza machozi  kwa kuwa hatuwajui, mwanzo huwa wana act kuwa wanapenda kisha anaanza kukusoma taratibu tabia na mwenendo wako akiona unamridhisha basi huuachia moyo wake katika penzi,  laa akiona kuna mambo hayamridhishi baasi ataanza kukuepuka taratibu. 

 Sasa wewe uliejipeleka sina uhakika kama ameshindwa tabia yako au kakuona wa kawaida.  Lakini kaa naye muulize taratibu nini hatma ya uwili wenu atakachokujibu basi patana nacho.



 Jamani mwanaume anayekupenda atakuja kwenu atajitambulisha na kutoa mahari kisha mnaoana.  

NIWATAKIE WEEK END NJEMA





Toa maoni yako

Friday, January 24, 2014

MAANA YA MWANAMKE



Sam wa Dar

Dada mi nina tatizo naomba usipendelee kwa kuwa mwanamke mwenzio,
mke wangu hapendi kupika wala kazi za nyumbani kila kitu anafanya housemaid, hata kama usawa wenyewe basi unashindwa hatakutandika ndani mwako, ukimwelekeza ana mdomo mchafu balaa.  Naomba unisaidie bahati nzuri na humu kwenye blog yako anaingia 


JIBU

Mmmh aibu ulimtoa wapi au ndio mlikutana baa ukaona anafaa, 
Wahenga wanasema ni bora ukosee kujenga nyumba kuliko kukosea kuoa.

Haya nawe mwanamke mwenzetu ulilelewa mbinguni au chini ya bahari? Mwanamke kutokujua kupika shost majanga tena  tukushushie bendera nusu mlingoti, we ni wa kike sio mwanamke, mwanamke hawezi kuwa hajui kupika, na kitanda utandikiwe khaaaa.

Nyie ndio mnaosababisha wasaidizi wanabakwa/wanabebeshwa mimba na waume zenu kisha mnawafukuza kwa taadhira, wanaenda makwao kuongeza mzigo wa umasikini, kumbe kosa lako mwenyewe.

Fahari ya mwanamke ndani ya nyumba usafi uujue, chakula cha mumeo bibi weye, chumbani  kwako ndio kabisa huyo maid hatakiwi hata kuchungulia, ukiambiwa mdomo na ndivyo walivyo wavivu wote mdomo silaha, waongo, chochote kwao sawa tuu,  kazi ni kuunga kucha na kuzitia kila aina ya  rangi sijui hata usafi wa maungo yao wanaufanyaje.

Kila siku unazusha safari ili usikae jikoni, saluni zote wanakufahamu aliyekwambia mwanaume anakula urembo nani, mapenzi sio kitandani tuu bali umjue mwanaume kula yake, vaa yake, apendavyo ufanye na anachokukataza acha, pia uwe mbunifu basi ndani ya nyumba kila mara unatakiwa um surprise mumeo kwa upambaji wa nyumba yenu. Badilika my dear maisha si lelemama hapo ulipo kuna wenzio wamepanga msitari  wanakusubiri utoke waingie.

Asikudanye mtu maisha ya ndoa yana heshima kwako na nyumbani kwenu.  Kama hufahamu kuwa mpole tafuta mtu japo umlipe akufundishe wajibu wa mwanamke  vinginevyo utawahesabu wanaume kama nguo.

Kila kitu msaidizi siku ukimkuta anakusaidia kitandani usihamaki kachukue pop corn  uangalie tv sebuleni uache muvi iendelee.
MAANA YA MWANAMKE NYUMBA

Bye

















Toa maoni yako

Thursday, January 23, 2014

NGUVU ZA ................... TALK ABOUT LOVE





Deo wa Moshi

Dada mi naomba unishauri  mi sio mwelewa sana wa mambo ya mapenzi, nina miaka 27,
nikiwa na demu wangu yaani naishia moja tuu mpaka kaanzisha ugomvi home kuwa nina demu mwingine, nifanyeje


JIBU
Pole kaka kwa matatizo hayo nasikitikita mbona ni kijana mdogo sana inakuwaje?
Hebu kama una mawazo punguza kisha onesha kujali uwapo kwenye majamboz, uambie moyo wako kuwa huyo uliyenae ndie alpha na omega huna mwingine unaempenda zaidi yake.
kisha jaribu kutumia muda kidogo katika maandalizi ya kuingia kwenye tendo,

Pia tahadhari na kuiga mambo ya porn kwani mwanaume mishipa ya nguvu za kiume ipo mwishoni na ni myembamba sana hivyo unapomruhusu mwanamke akunyonye akitumia meno huwa anakata ile mishipa taratibu mwishowe unakuwa mbete mbete.

Pia kinywa au sehemu ya nyuma ina joto kali sana kuliko ilivyokadiriwa na Muumba hivyo kama ukijizoeza hizo sehemu mbili kutumia basi una hatari ya kupoteza nguvu mapema sana kuliko unavyotarajia, na hata ukimwingilia demu sehemu ya kawaida basi hutahisi raha yoyote na kusababisha usifunge magoli ya haja.

Pia chakula jamani kinachangia sana kupoteza nguvu za kiume, hebu jaribu kula full diet uone, achana na vihepe au mkate hebu kama inawezekana, kisha penda kutafuna muhogo mbichi na karanga mbichi kama demu wako hajakukimbia.

Tafadhali usijaribu kunywa madawa hovyo yatafanya tatizo liwe kubwa badala ya kupungua.
ni hayo tuu. 

taa taaa











Toa maoni yako

Tuesday, January 21, 2014

KWANINI HATUWEZI KUISHI BILA MAPENZI

Habari za long weekend nadhani inaendelea vyema samahani kwa kukosa mada siku zilizopita ilikuwa ni nje ya uwezo wangu, nimerudi sasa naomba  tuendelee

KWANINI HATUWEZI KUISHI BILA MAPENZI

Mwanzo kabisa nilisema mapenzi yana roho yanaishi kama kiumbe hai, kwa sababu hebu fikiria mara ya kwanza unapopenda huwa unakuwaje, 
kisha kadiri siku zinavyoendelea inakuwaje 
na je penzi likifa ghafla inakuwaje

Hivyo ni kawaida ya kiumbe chochote chenye uhai kuwa katika mapenzi si wanadamu tuu hadi wadudu warukao na watambaao.
Naweza kusema ni mpango wa Mungu kwa kweli, kwani mtu yeyote asipokuwa katika mapenzi hujiona na mapungufu flani yaani kama hujielewi au dunia imekutenga kama hivyo.
Hata kiafya na kiakili pia mapenzi yanahusika kukufanya uwe na akili timamu na afya njema huwezi kuumwa hovyo hovyo mara kiuno au nyonga kwa wanawake.

Pia mtu anaposalitiwa huumia sana na kuiona dunia chungu hata kama ana mali na fahari vyote kwake si kitu hupelekea kujiona hafai tena mbele ya jamii  mpaka kufikia kujidhuru au kumdhuru mpenzi wake.

Pia hata kama ana  kisomo, cheo, au familia inamtegemea kiasi gani kwake huwa haina maana kama ameumizwa kwenye mapenzi.

Mapenzi yanaweza mbadilisha mtu tabia mpaka watu wakamshangaa  mfano labda alikuwa mwenye roho nzuri kwa familia na jamii baada ya kuingia kwenye mapenzi misaada na ule upendo aliokuwa anauonyesha kwenye familia hufa, akawa anamsikiliza mpenzi wake tuu.

Mapenzi hupelekea wengine kukosa radhi za wazazi wao, kugombana na ndugu zao mpaka wakashindwa kuzikana.

Mapenzi hufanya watu wakafukuzwa kazi, wakahama kila nyumba, wakashindwa kuishi na majirani vyema, wakawa na maadui wengi katika jamii.

Juu ya yote hayo bado watu wakaendelea kupendana bila kujali yote hayo.

AMA KWELI MAPENZI NI KITENDAWILI

Mpenzi msomaji wangu nadhani leo tumemalizia maswali yote niliyoyauliza kwenye somo letu la kwanza kabisa kuhusu mapenzi.

Naomba uhai na uzima ili tuendelee na mambo yahusuyo mapenzi mi si mjuzi sana ila napenda kushare nanyi nikijuacho kuhusu MAPENZI.
Tchao




Toa maoni yako

MASWALI YENU - TALK ABOUT LOVE







Assalaam alaykum 

Samahani kwa kuto onekana kwa sababu ambazo zilikuwa nje ya uwezo wangu.

Leo nitawaletea maswali ya wasomaji wangu kama walivyoniandikia, ila itifaki itazingatiwa sitatoa picha wala address ya muhusika bali jina la mwanzo tuu.

Jane wa Arusha:
Habari dada  mimi nimefuatilia sana mada yako humu nimepata uelewa sana ahsante dada Mungu akubariki.  Sasa swali langu linakuja hivi
mimi nina mume wangu tuna miaka 3 hajawahi kuniridhisha kimapenzi na wala hajali akimaliza yeye basi anaendelea na mambo mengine au kama ni usiku anakoroma dada nifanyeje?

Jibu
Tatizo hili lipo wanawake wengi wanalalamika, wengine wanafikia hata kutoka nje ya ndoa zao jamani sijui kwanini baadhi ya wanaume ni wabinafsi sana wakisharidhika basi utafikiri alikuwa na toy.
Jamani wanaume mnaopitia humu jiangalieni sometime mnavunja mapenzi na ndoa zenu wenyewe, mwanamke atakupendaje wakati humridhishi acheni mfumo dume.

Kwanza sijafahamu ilikuwaje mpaka kufikia hatua ya kufunga ndoa, pili hujaniambia umri wako ni miaka mingapi, 
Kama mlianza mapenzi kabla ya kufunga ndoa ina maana hilo suala hukulipa umuhimu, kwa sababu tamu ya chai sukari, kama mwanaume ni mbinafsi kitandani wa nini sasa.  Utaishije ndani ya ndoa bila kufurahia tendo  wakati ndilo linalomfanya mtu apende kupita kiasi.

Pia wakati wa tendo unatakiwa mawazo yako uyahudhurishe hapo na uhisi kila tendo analokufanyia mpenzi/mume wako linakufurahisha, kama kuna sehemu akikushika unahisi raha basi ni vyema kumwambia, au anakuumiza pia sema ili uweze kufurahia.  Na kama bado hujawa tayari mwambie we bado hujakiona kituo. Pia maandalizi yawe mazuri unayofurahia sio anakoshika siko unakojisikia na akitaka kufanya haraka we macho makavu mwambie  aendelee na romance kwani hakuna raha kama hujalewa na romance maana utachunika na kulichukia tendo. Matokeo yake utakuwa unamtazama jicho kali sura umeikunja kama uko vitani.  haaahaaa inakuwa kashda tena, ukitoka hapo umeumia kama umebakwa.

Pia je msitu umefyeka? kwa wote wawili maana kama mmoja wenu anao mmh shost msitu unakata kuliko wembe hivyo ni muhimu sana kusafisha msitu 

Jambo lingine umri kisaikolojia mwanamke kuzama kwenye mapenzi, kujua thamani ya penzi,  akahisi raha, umakini, akafurahia tendo, akalia ki kweli kweli kwa raha ni kuanzia miaka 30-35 na kuendelea iwapo atakuwa na mwanaume anaye yajua mapenzi  haswaaaa.
Vinginevyo  mmh. 

Ok tuonane kwa swali jingine 

Tchao














Toa maoni yako

Friday, January 10, 2014

ZANZIBAR

Napenda kuungana na Wazanzibar katika kusherehekea miaka 50 ya MAPINDUZI YA ZANZIBAR

 Leo naomba niwape vitu vya Zanzibar ambavyo sehemu nyingine ni adimu kuvipata.
Kwanza wazanzibari ni wakarimu na waaminifu sana ukipata tatizo hukuhudumia kama mnajuana tangu zamani.

  • USAFIRI
Usafiri wa kuingia na kutoka Zanzibar ni wa anga na bahari tuu
  • MAVAZI

        Katika Tanzania nzima hakuna sehemu wanawake wanavaa mavazi ya aina moja kama Zanzibar inapelekea hata wageni kuiga mavazi ya kujistiri mwili.  wenyewe huitwa utamaduni wa mzanzibari.

  • SITTING ROOM
wazanzibar hupenda kuweka mazuria na mito tu hivyo kama hujui kukunja miguu utaondoka kabla ya wakati.

Hotel iliyoko katikati ya bahari inasemekana ni hotel ya kwanza duniani.


  • DORIAN
hili tunda  linanuka sana kiasi ukilibeba popote ukipita lazima watu wajue kama unalo, lakini ni tamu sana wenyewe hula hata kwenye chakula, wengine wakimaliza kulila hupiga mswaki.





wageni wakifurahia vyakula Forodhani

  • FORODHANI
Hii ni sehemu nzuri sana katika Tanzania hakuna mahali pazuri kama hapa 
kuna vyakula vingi vya kizanzibari vitamu,
 hapachagui mwenye nacho au hana 
hapana kiingilio wala hulazimishwi kununua
huenda kila rika hapachagui wazee, vijana au watoto, wageni au wenyeji
wazanzibari hutumia sana mahali hapa kubarizi au kupunga upepo baada ya pilika za kutwa nzima.


Haya haya hivi ni baadhi ya vitu nilipenda nawe uvielewe.

MAPINDUZIIIIIIIIIIIII
DAIMAAAAAAAA




Thursday, January 9, 2014

Nani anastahili kupendwa? TALK ABOUT LOVE

Hellooo
wapendwa wasomaji wangu natumaini weekend ilikuwa poa mi pia kwangu ilikuwa shwari 
tuendelee...........
NANI ANASTAHILI KUPENDWA?
Nadhani wote tuna jibu moja kuwa wote tunastastahili kupendwa, jamani kupendwa raha sana asikwambie mtu, hujiona uko kwenye ulimwengu wa peke yako moyo unachanua kwa furaha.

KWANI KUPENDWA NI NINI
Ni kule kudekezwa, kupendelewa, kuchaguliwa, kubembelezwa kama mtoto, n.k.

KWA NINI UPENDWE?
Hapa sasa majibu yake lazima yawe tofauti
kwani kila mtu ana sababu iliyomfanya apendwe, na kama kungekuwa na sababu moja au mbili basi kuna watu wangekufa bila kupendwa.

Unaweza kupendwa kutokana na 
  1. Tabia yako njema 
  2. uzuri wako sura au umbo
  3. umaridadi wako katika uvaaji au mazingira unayojiweka
  4. ucheshi wako 
  5. sauti yako 
  6. umaarufu wako n.k.
Kwa upande wa wanaume wenye akili asilimia nyingi hupenda tabia, yeye anaweza kuwa malaya kweli kweli anachezea watoto wa watu kama aliwaumba yeye lakini akitaka kuoa anatafuta mwanamke mwenye tabia njema.

KWANINI
kwa sababu mwanaume mwenye akili anajua kuwa kuoa ni kuanzisha familia na ukoo sasa ili familia iwe na sifa nzuri katika jamii basi lazima apate mke bora, mwenye tabia njema.

Sio mke asiyejijua yeye ni nani ndani ya nyumba, siri za ndani anamuhaditia hadi mfanyakazi wa ndani tena usikute mdogo ki umri, nyumbani kwake akiwepo sawa asipokuwepo wala hakuna tofauti, kisha utake kupendwa utasubiri sana.

JE UNAJUA KAMA UNAPENDWA?
Labda tuseme ndio, je unajua anachokupendea? Au ili mradi tu ukiletewa zawadi, au akikuchekea  basi mwenyewe unaridhika kuwa unapendwa?
Chunguza vitu gani anapenda wewe uvifanye, na ni rahisi tu mfano:-
Chakula ukipika wakati wa kula muulize- vipi chakula kizuri eeh?  majibu yake yachunguze anaweza akajibu kwa mmh, au ndiyo, au naye akauliza kwani kapika nani, na utakapo mjibu ni wewe basi anaweza kukushauri cha kuongeza au kupunguza. Au akakifurahia sana chakula, akakisifu kuwa kizuri.

asikudanganye mtu uchawi wa kwanza wa mwanamke kwa mumewe/mpenziwe ni mapishi, mnapoteza pesa bure kwa waganga wa kienyeji dawa unayo mwenyewe.   Mapishi bi dada leo umepika hiki kesho kile, sio kila siku mchana ugali usiku wali mmh na mapishi ndio yale yale akipata wa kumbadilishia mlo kwako bai bai.
Maandalizi ya chai, tena  chakula cha asubuhi wengi sana tunafeli, mwanaume umekazana kumlisha vitafunwa vya kununua kama maandazi, chapati,mkate bajia n,k.
Hivi we kupika huwezi kweli, haya siku za kazi zinajulikana weekend je, mnashindana kulala mpaka msaidizi akugongee chai tayari, je ungeamka mwenyewe ukaiandaa kisha ukamkaribisha mumeo kwa sauti nyororo ataacha kukupenda kweli?
Kingine usafi jamani mwanamke barabarani alivyojipamba kama mdoli, mmh nenda kwake hasa chumbani hapafai, ukimuuliza atasingizia muda hana lakini wa kukaa kujipamba kwenye dressing table saa nzima anao. Au ndio msaidizi ataitwa afagie adeki chumbani kwako mwanamke looh kesho ukimkuta kitandani na mumeo toka taratibu ukashushie juisi.

Haya usafi mwingine wa mwili na huu ndio wengi wetu sijui hatuujui au ndio makusudi,  mwanamke unayejua maana ya usafi utaweka makucha kama shetani vidole vyote utajisafishaje?  Au ndio toilet paper hapana mwanamke yake maji bwana, wanawake tuna vumba afadhali ya samaki sangara, usipojua kujisafisha utasema una nuksi, kwani mwanaume atakufuatilia kwa mbwembwe akishafanya ngono nawe mara moja tuu hana hamu na wewe tena, na alivyokuahidi atakufanyia vinaishia hapo hapo.
hakupendi tena.

Kingine jamani mautundu kunako majambo wote lazima muwajibike na mfurahie lile tendo, hasa mwanamke kila mara  unatakiwa uwe na utundu mpya, hata chakula kila siku ugali maharagwe jamani si atavimbiwa.
utapendwa kweli.
mmh mengine tuulizane pole pole jamani  humu hapafai.

KWA WANAUME.
asilima nyingi wachafu, wabishi na wabinafsi sana.

UCHAFU
Mwanaume na mazingira ya usafi ni wachache sana wanaoweza, kwani ule mfumo dume unawaumiza sana. utotoni alikuwa anafuliwa nguo ananyooshewa, akirudi shule anatupa uniform dada yake kama anaye au msaidizi wa ndani aokote akafue na wengine walikuwa wanafuliwa na mama zao.

Sasa wakioa mwendelezo unakuwa vile vile, usipomwangalia anaweza soksi akavaa tuu mpaka zikanuka kama anatembea na maiti ya panya.  Shati siku mbili tatu analo tuu, wengine hata nguo ya ndani umfulie laa sivyo atavaa tuu.
Mwanamke kama alisafiri akija rudi badala ya kupumzika na uchovu wa safari atafikia usafi na uchovu wote utaisha jinsi chumbani atakavyo pakuta.
Hamu na mapenzi aliyokuja nayo mwanamke huyu yote yanaisha, halafu akupende never.

Kero ndani jamani kuna wanaume wana gubu ndani ya nyumba mpaka chefu, kadogo linakuwa kubwa, mwanaume anasema kama kafungwa kaseti looh, la chumbani mpaka nje watasikia, mbele ya wageni, watoto, wasaidizi ye ni kufoka tuu.  Sijui ndio ajulikane Mkuu wa kaya mi hata sijui kwa kweli kujifanya Mungu mtu ndani ukiingia watu wote amani hawana mapigo ya moyo yanawaenda mbio kama wamekutana na mtoa roho.
Haaa we mwanaume mwenye tabia hii utangoja sana kupendwa.

UBINAFSI
Jamani mapenzi ni kueleweshana nishike hapa ukifanya hivi mwenzio naliwazika, wanaume wengi hawapendi kueleweshwa utamwona anajiliwaza yeye tuu akimaliza hana habari kama na mwanamke ni binaadamu hupenda aliwazwe na kufika kileleni kama mwanaume.  Ole wako umwambie  hakawii kukuita malaya sijui haya mapenzi waliumbiwa wao tuu.  Hali hii humsababishia mwanamke akose furaha na atafute mtu wa kumliwaza.  Kisha we unategemea upendwe na mwanamke huyu itakuwa ngumu.

UBISHI 
yaani mfano mkeo  kakuandalia nguo za kuvaa, viatu soksi, tai kaweka tayari, asubuhi we unavikataa na kumuamsha akutayarishie vingine.  Hata mbele za watu anaweza kuongea neno we ukampinga tena kwa dharau mpaka akaona aibu, ndio utakuta wanawake wengine wanakuwa wakimya akiwa na mumewe mbele za watu sio anakosa cha kuongea anaogopa kushushuliwa.  Mara nyingi haukubali ushauri wake hata kama una manufaa kwenu kisa ni mwanamke,  mmh kupendwa hapa ngumu.

Mmh hili somo ni pana sana lakini huwa ndio kitovu cha amani ndani ya nyumba au chanzo cha migogoro vile vile.
Nikushukuru wewe ulietumia muda wako kuperuzi hapa nadhani kuna moja au mbili umepata bila shaka na kama una nyongeza tafadhali niandikie kwenye USHAURI/MAONI au nipigie kwa namba hizi 
0712 244 221
kwa leo tuishie hapa wapendwa niwatakie Jumatatu njema.















Friday, January 3, 2014

Nani anastahili kupenda? - TALK ABOUT LOVE







Ni siku nyingine tena wapendwa wasomaji wapendwa, natumaini mu wazima.  

NANI ANASTAHILI KUPENDA?
Unapoingia kwenye mahusiano lazima ujiulize swali hili, maana wengi wetu hupenda kulaumu upande mmoja yule hata hanipendi.
Sote tunastahili kupenda tena kwa moyo na ndio maana hata mbele ya za watu unapotaka kufunga ndoa ya aina yoyote ile lazima uulizwe kama umempenda na uko tayari kuwa nae.  Na hakuna sehemu hata kwenye vitabu vya Mungu palipoandikwa alazimishwe mtu kupenda, huwa ni baadhi ya mila na desturi tena zamani siyo sasa sidhani kama taratibu hizi bado zinafanyika.  Kwanini suala hili hata Mungu hakutaka lilazimishwe?
Kwa sababu bila kumpenda hutaweza kuishi naye kwa amani. Na kama kukikosekana amani ndani basi jua:-

  •  hamtaweza kuwa na maendeleo kwani hamtaweza kushauriana kila mtu atakuwa na lake.
  • mtasumbua vizazi vyenu kwani hamtakuwa na sheria ya pamoja jinsi ya kulea watoto wenu.
  • kama mwenzio ana mapenzi ya kweli  atateseka kwa sababu hatapata upendo mzuri kutoka kwako.


Hivyo epuka sana kuingia kweye mahusiano bila ya kuwa na mapenzi ya kweli kwani yatakutesa hata na wewe mwenyewe hutakuwa na furaha, matokeo yake kila mtu anatafuta mpenzi wa nje wa kumpa furaha, mnabaki ndani ya nyumba mnaishi kama jela, karaha mtindo mmoja.

Katika suala hili la kupenda mara nyingi wapendaji na wanaume, kwani wanawake hupata fursa ndogo sana ya kupenda na kuishi kwenye pendo.  Kwa sababu katika mila za kiafrika mwanaume ndie anaetafuta anayempenda na akimpata hasiti kumwambia.  
mwanamke yeye hata kama akimpenda mwanaume hawezi kumwambia,  na hata akisema asilimia kubwa huishia kudharauliwa na kuonekana ni malaya, pia mwanamke kaumbwa na aibu hasa katika masuala ya mapenzi.
Hivyo hata kama anapenda masikini huishia kuonyesha upendo, ukaribu, ucheshi, huruma kwa yule ampendae bila kuwa na matumaini kama hayo ayafanyayo yatakidhi matakwa yake.
Mwanaume nae akiona unamfanyia hivyo basi kama hana imani hujidai anakupenda akishafanya ngono nawe, anakutupa huko bila kujali atakuumiza namna gani.   Wengine hufikia hata kukutangaza mbele za watu kuwa wewe ni malaya unayejitongozesha kwa wanaume, kumbe masikini ulikuwa na upendo wa kweli kwake.

Baada ya kutendwa  mwanamke huyu atakacho ona bora kwake ni kugawa dozi ya maumivu kwa kila mwanaume atakaye jileta kwake, matokeo yake anakuwa malaya kweli wakati mwanzo hakuwaza wala hakutaka kuwa hivyo.
Kwa mwanaume naye vile vile tena wao ndio wanaumia sana.

kwanini?
kwa sababu wao wanahangaika kutafuta mwanamke ambaye anampenda, katika kutafuta huko hutumia pesa, zawadi mbali mbali, kumtoa matembezi ya jioni, kutafuta maneno ya mapenzi ambayo yatamvutia huyo mwanamke ili amkubali, hubadili muonekano wake ili aendane na huyo ampendaye, wengine hufika hata kukodi mavazi, magari kujiongopea anaishi sehemu nzuri au kazi yenye hadhi ili tu ampate ampendae.

Na hili la kuongopa linawaharibia wanaume wengi sana akimpenda mwanamke eti kuna msemo kuwa huwezi kumpata mwanamke mpaka umwongopee, 
Wewe usijidanganye kwani inawezekana kuwa kabla hujamtamkia huyu mwanamke unampenda yeye pia alikwisha kukupenda.   Hivyo ukimtamkia hufurahi moyoni kuwa njozi zake zimetimia kwa kumpata ampendae.
Sasa ukianza kumuongopea madai yako ili akupende ndio unaharibu kabisa kwani akigundua utakuwa adui yake namba moja.  Utamkosa na kujuta lakini ndio hivyo tena majuto ni mjukuu.

Hivyo kupenda ni kwa kila mtu anatakiwa ampende mpenzi wake, na awe mkweli  sio kujitapa ooh nimesoma Marekani na Canada, nina DEGREE NANE,MASTER  SITA, PHD,  jamani mapenzi na hayo mavyeti yako wapi na wapi. 
 Mie nikiwa nawe hutojuta nina nyumba nane nimepangisha wazungu magari ya kifahari, harusi yetu tutafunga angani, wakwe nitawapeleka UK shopping, wewe ndie utakuwa msimamizi wa mali zote hizi, hebu sema unataka nini tena. Hee unaoa mke au supervisor?  Ingawa si vibaya lakini isiwe ndio kigezo cha kukubaliwa. 
 Hivi mapenzi yangeendana na utajiri, masikini si angekufa bila kutongoza, asikudanganye mtu mapenzi hayachagui kisomo wala pesa, yule aliyekugusa moyoni ambae ukimuona moyo unawaka kwa furaha na usipomwona hujihisi ugonjwa usio onekana hospital zote, basi huyo ndie anastahili uwe nae. Na ndio unastahili kumpa mapenzi yako ya dhati.

kwa leo nitaomba niishie hapa,

kwa maoni/maswali/ushauri niandikie kupitia mkono wako wa kulia pameandikwa MAONI/USHAURI itakuwa siri yetu na nitakujibu kwa njia hiyo hiyo ya email.
AHSANTENI


Thursday, January 2, 2014

Hivi kuna Mwalimu wa Mapenzi? - TALK ABOUT LOVE

Assalaam alaykum wapendwa, 
Habari za mwaka mpya natumaini wengi wetu tumesherehekea kwa amani na utulivu.
Haya ni siku nyingine tena tunaendelea na mlolongo wetu wa safari ya mapenzi na leo, tunataka kumjua nani mwalimu wa mapenzi.

HIVI KUNA MWALIMU WA MAPENZI 
Asilimia kubwa ya wengi wetu ukiwauliza swali hili, hujibu hakuna shule ya mapenzi.
kwa upande mwingine wapo sahihi kwani ni kweli hakuna shule iliyo sajiliwa rasmi kwa kufundisha mapenzi.
Pia hudhani mapenzi ni ngono, wakati hilo tendo huwa ni sehemu ya mapenzi.

Haya basi mwalimu ni nani?
Mwalimu wa kwanza ni 
  1. Moyo wako
  2. jamii

MOYO
kwanini moyo?
Kwa sababu moyo unapopenda huwa ni mwalimu mzuri sana kwani
hukufundisha jinsi gani 
utabasamu ukiwa na mpenzi wako
 maneno gani umwambie
sauti gani utumie
na kingine ni muonekano uvaeje ili akikuona ataharuki 
haya huwa mwalimu wake ni moyo kutokana na jinsi gani unavyompenda,
Ingawa sio wote wanaojali ushauri wa moyo.

JAMII
Pia ni mwalimu mzuri sana wa mapenzi, kwa sababu utasoma kwa 

  • Kukopi kutoka kwa wazazi labda ulikuwa unamuona mama/baba anamfanyia nini mwenzie.  Na ndio maana ukipata mwanaume ambaye baba yake alikuwa mpigaji,mtukanaji asilimia kubwa naye huwa hivyo hivyo.
  • Majirani, Marafiki, kusoma majarida mbali mbali blog kama hivi inasaidia sana kuona kipi uchukue ambacho kitafanya mapenzi yenu yasonge mbele.
  • Kuna makabila ambayo hutoa mafunzo kwa lugha ya kibantu huitwa "unyago, kuchezwa, Ngoma au kwa kule kwetu huita msondo, kwa wanaume "Jando".   
Kusema kweli mafunzo haya yalisaidia sana kudumisha mapenzi na ndoa kwa ujumla, kwani waliokuwa kwenye mapenzi kila mtu alijua wajibu wake na mipaka yake katika mapenzi.
kwa sababu walengwa hujifunza jinsi ya kuishi na wenza wao, na malezi ya familia.
Ingawa mafunzo ya baadhi ya makabila yana dosari kama kufundisha wanawake kuwa na wanaume zaidi ya mmoja lakini asilimia tisini yana faida sana na ndio maana ndoa za wazazi wetu zilidumu na nyingine zimendeleea kudumu mpaka leo.

Tofauti na sasa mtu mpaka anaoa/anaolewa hajui chochote zaidi ya tendo la ndoa, utakuta   mkaka au mdada anaongea siri za ndani za mpenzi wake mbele ya marafiki, wafanyakazi wenzie, n.k. Mdada huyo sasa utamkuta anajifaragua,
  •  "Mie mpenzi/mume wangu ananipenda, mara kasema mwezi huu ananinunulia gari,
  •  likizo hii tutasafiri kwa ndege,
  •  nimemwambia abadilishe zile samani ndani wiki ijayo shost ukija utakuta mambo mapya,
  • Kwangu hafurukuti nimemweka kiganjani, niseme nini asitende
  •  kuna dili anafuatilia hilo la mamilioni shost akipata tu namwambia aninunulie nyumba.
 Tena anaona raha wenzie wanavyomsikiliza hajui sometime  anahatarisha hata maisha ya mpenzi wake. 

Mkaka nae
Duh washikaji demu wangu nampenda naye ananipenda sana, yaani nikimkumbuka kazi haziendi wangu, mtoto anajituma kitandani ile mbaya, kwanza alivyo hata nikitembea naye najiona kama sienei vile, halafu sasa kwao kuna pesa yaani hata ukimpa pesa hapendi anarudisha, ameshasema nikiwa na shida nimwambie atanipa kwani ana account tangu mdogo halafu hata hajaanza kuzitumia.

 Hivi nyumba ilivyojengwa ikakatwa vyumba, kukawekwa mlango na madirisha ilikuwa kwa sababu gani?wewe ambaye mambo yako ya chumbani unayaanika kama samaki ng'onda.

Halafu kesho unagombana ooh rafiki yangu kanichukulia mpenzi wangu, si umemchuuza mwenyewe kama nguo mnadani
Yote haya ni kukosa mafunzo, mwenye mafunzo huwezi kumkuta ana haya mambo
Au wengine akikosana na mpenzi wake watu wote wanao mzunguka watajua, jinsi atakavyojitapa na maneno ya kashfa 
  • Oh yule bila mimi asingekuwa vile, 
  • Kwanza nimemsomesha, wazazi wake masikini mimi ndie niliyekuwa nawahudumia
  • Alikuwa hajui hata kuvaa 
  • Kwanza hajui usafi nilikaa naye basi tu
  • Muda wote sikuwa hata na raha bora tulivyoachana
  • Hivi yule nae mwanaume/mwanamke kweli wakiitwa wa aina yake nae atatoka
  • Mtu gani asiye na fadhila.
Na mengine mengi mpaka kutoleana siri za maungoni, ili iweje, unapata faida gani, unao waambia wakishajua wamfanye nini?

Mpenzi msomaji wangu, sababu 
Ni kuingia kwenye mapenzi bila kuyajua hasa wanawake, kisha unakuwa kichwa cha umbea mtaani, wakikuona tu wanakuita kwa bashasha ili uongee ya kwako, wengine watakupa ushauri mbaya unajikuta unaanzisha migogoro ndani isiyo na kichwa wala miguu, unaondoka kwenye ndoa yako na kuwaacha watoto wanateseka, kisha alokushauri uondoke ye ndie anakurithi. 

Wengine wanakushauri kwenda kwa waganga wa kienyeji

Aliyekuambia kuna dawa ya mapenzi nani?  
Kwa mganga  unapewa dawa kamuwekee kwenye chakula mumeo matokeo yake anakuwa zuzu, kila utakachofanya anakuangalia tuu, hana ushauri ndani, majukumu ya kulea familia yanakukabili peke yako kwani ye hata kumkanya mtoto hawezi anakusukumizia wewe, unaanza kulalamika tena mitaani kuwa hakusaidii majukumu, na wakati ulipokuwa unamwambia mganga "nataka afunge mdomo wake, mimi ndio niwe mwenye sauti, na kila ninalomwambia atii,"  
si kanyamaza sasa uone familia inavyokuharibikia hivi hivi unaiona.

Dawa ya mapenzi ni ulimi na uhodari wako katika kufanya yale yanayomfurahisha mpenzi/mume wako.
Hiyo midawa mnayopewa ni kuwatafutia maradhi tuu watoto wa wenzenu.
Na yote hii hutokana na kutopenda kuambiwa kweli, ukikosea hutaki kuomba msamaha, unalotaka lazima lifanyike, kutaka wewe ndie uwe mwenye sauti kuu ndani ya nyumba, mwenzio ashindwe hata kuwasaidia wazazi wake.  Huu ni ushetani mkubwa sana unachangia sana kuvuruga familia.

Naomba niishie hapa kwa leo,
Wapenzi Wasomaji wangu nimepokea maswali yenu, maoni ushauri nawashukuru sana kuona ninachojitahidi kukidadavua hapa kwa kiasi kikubwa naeleweka.  
Endeleeni kunitumia na ipo siku nitayajibu hapa hapa bila kutaja majina wala email zenu.

ahsanteni sana tuonane mada ijayo